Jumatano 2 Septemba 2026 - 10:27
Umoja wa Waislamu Utarejesha Heshima na Nguvu Yao

Hawza/ Sheikh Ibrahim Zakzaky, kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria, amesisitiza umuhimu wa umoja na mshikamano wa Umma wa Kiislamu, akisema: “Umoja wa Waislamu ndiyo njia ya kurejesha heshima na nguvu yao.”

Kwa mujibu wa taarifa ya Idara ya Kimataifa ya Shirika la Habari la Hawza, Sheikh Ibrahim Zakzaky, mbele ya idadi kubwa ya Waislamu kutoka maeneo mbalimbali ya Nigeria, alitoa hotuba katika hafla ya kuadhimisha kuzaliwa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w.), na kuhitimisha maadhimisho ya Wiki ya Umoja wa Waislamu mjini Abuja.

Kiongozi huyo wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria, katika hotuba yake akirejea maadili mema na matukufu ya Mtume wa Rehema (s.a.w.w.), amesema: “Mtume kwa maadili yake mema aliwashinda maadui zake,” huku akikumbusha kuhusu msamaha, upole, rehema na kusamehe kwa Mtume (s.a.w.w.), hata dhidi ya wale waliomdhuru Mtume huyo.

Ameongeza: “Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w.) anapaswa kuwa alama na kipimo cha maadili na mwenendo mwema kwa Umma wa Kiislamu.”

Sheikh Zakzaky katika kuendelea na hotuba yake amesisitiza ulazima wa kuwepo kwa umoja miongoni mwa Waislamu, akisema: “Udhaifu na hali ya kubaki nyuma ambayo Waislamu wanakabiliwa nayo inahusiana na kutawanyika na kugawanyika kwao.”

Amewataka Waislamu waungane na kuwa na mshikamano kwa ajili ya maslahi ya Uislamu, akisisitiza kwamba umoja wa Waislamu unaweza kurejesha heshima na nguvu yao; jambo ambalo maadui wa Uislamu hawalitaki, kwa sababu kugawanyika kwa Waislamu ni kwa manufaa yao.

Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria, mwishoni mwa hotuba yake, huku akieleza matumaini yake kuhusu mustakabali wa Umma wa Kiislamu, amesema: “Hali ya sasa ya Waislamu itakwisha, dini itaimarika na kubaki imara, na nguvu pamoja na heshima ya Umma wa Kiislamu, Inshaallah, vitarejea.”

Hafla hiyo ilifanyika mjini Abuja katika mfumo wa programu za Wiki ya Umoja wa Waislamu, huku iliambatana na kumbukumbu ya kuzaliwa Mtume Mtukufu wa Uislamu, Muhammad Mustafa (s.a.w.w.), pamoja na Imam Ja‘far Sadiq (as).

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha